Safari ya Miaka 30
Kwa mujibu wa Dkt. Alfred Elias Kimonge, Katibu Mkuu wa CBT, mchakato wa kutafsiri Biblia hiyo ulianza mwaka 1994 baada ya maombi kutoka kwa Makanisa ya Iringa. Mradi huo ulisimamiwa na Chama cha Biblia Tanzania kwa kushirikiana na makanisa mbalimbali, wataalamu wa lugha, wahakiki, watafsiri, na wadau wa ndani na nje ya nchi.
Dkt. Kimonge alibainisha kuwa tafsiri ya Agano Jipya ilikamilika mwaka 2004 na kuzinduliwa rasmi mwaka 2008. Tafsiri ya Agano la Kale ilianza mwaka 2009, na sasa Biblia kamili imekamilika na kuzinduliwa rasmi leo tarehe 29 Juni, 2025. ‘‘Biblia inayozinduliwa leo inapatikana katika matoleo mawili: toleo la Kiprotestanti lenye vitabu 66, na toleo lenye vitabu 72 lijulikanalo kama Deuterokanoni, linalofaa zaidi kwa matumizi ya Makanisa ya Kikatoliki (TEC),” aliongeza kusema.
‘‘Tunamshukuru Mungu kwa kuona siku hii. Hii ni ushuhuda wa kuwa Neno la Mungu linaweza kufika katika kila lugha, kwa kila mtu,” alihitimisha Dkt. Kimonge.