Mkutano Mkuu wa Mwaka (AGM) 2024
Wasiliana
Phone
(+255) 784-683 120
Location
9th Road /14 Hatibu, Madukani Area
(+255) 784-683 120
9th Road /14 Hatibu, Madukani Area
Mahali: ukumbi wa Nazareti, wilayani Gairo, mkoani Morogoro.
Hafla hii ilihudhuriwa na viongozi wa dini na serikali wakiwemo wawakilishi kutoka ofisi ya Mkuu wa (W) ya Gairo pamoja na ofisi ya Mkurugenzi mtendaji pia Afisa mipango na Afisa maendeleo ya jamii ambapo waliwapongeza sana wahitimu kwa juhudi zao kubwa na kusisitiza umuhimu wa elimu katika maendeleo ya jamii.
Chama cha Biblia, kupitia mradi wake wa Literacy for Women in Africa, kimefanikisha hatua muhimu katika kuimarisha elimu ya wanawake nchini. Mahafali ya saba ya mradi huu yaliyofanyika tarehe 23 Januari 2025 katika ukumbi wa Nazareti, wilayani Gairo, mkoani Morogoro, yaliwahitimu wanawake 353 katika ngazi ya A ya kusoma na kuandika.
Mradi wa Literacy for Women in Africa umeleta mabadiliko makubwa katika maisha ya wanawake hawa. Wengi wao sasa wanaweza kusoma Biblia, kuendesha biashara ndogo ndogo, na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii zao.
“Shuhuda kutoka kwa mmoja wa wahitimu: “Kabla ya kuanza kusoma, nilikuwa tegemezi sana. Sasa naweza kusoma na kufuatilia habari, na hata kuandika barua ya maombi ya kazi na kushiriki na mambo mbalimbali ya kijamii kama kupiga kura na kuchagua viongozi na hata kugombea nafasi za kiuongozi kama uenyekiti wa mtaa. Maisha yangu yamebadilika kabisa!”
Mahafali haya yamekuwa ushahidi tosha wa kwamba elimu ni nguvu. Chama cha Biblia kinaendelea kujizatiti kuhakikisha kuwa wanawake wengi zaidi wanapata fursa ya kujifunza na kukuza uwezo wao. Tunawashukuru sana wadau wote kwa ushirikiano wenu katika kufanikisha mradi huu.
Mahali: Kijiji cha Nyakimwe, Wilaya ya Buhigwe
Dhehebu: Kanisa la Anglican
Maelezo ya Meneja wa Tafsiri, Leah Kiloba
Leah Kiloba alielezea maendeleo ya mradi huu, akisisitiza kuwa Chama cha Biblia kinaendelea kujitahidi kuhakikisha upatikanaji wa Biblia kwa watu wote wa madhehebu mbalimbali bila ubaguzi. Alifafanua kuwa mradi huu unalenga kumjumuisha kila Mkristo kwa kutoa nafasi sawa ya kusoma Neno la Mungu katika lugha yao wenyewe.
Sherehe ya uzinduzi wa tafsiri ya Biblia ya Position ya Kiha (kitabu cha Yeremia) ilifanyika katika Kanisa la Anglican kijijini Nyakimwe, wilaya ya Buhigwe. Tukio hili lilihudhuriwa na waumini kati ya 400 na 700 kutoka madhehebu mbalimbali, pamoja na makanisa ya Anglican, Roman Catholic, Pentecostal, na Sabato, ambayo yalialikwa rasmi kushiriki.
Historia ya Mradi kutoka kwa Mchungaji Ntakije
Mchungaji Ntakije aliwasilisha historia ya mradi huu wa kutafsiri Biblia kwa lugha ya Kiha, akielezea hatua zilizochukuliwa kufanikisha kazi hii muhimu na changamoto zilizokabiliwa. Alielezea jinsi jamii imekuwa mstari wa mbele katika kuunga mkono mradi huu.
Kusoma Maandiko na Baraka za Ibada
Tukio lilihusisha kusoma maandiko kutoka kitabu cha Yeremia, sura ya kwanza, mistari ya kwanza hadi wa kumi, ambayo ilisomwa na mtafsiri Ahabu Ntibakanzi. Kabla ya kusoma, mchungaji Daniel Nzaino alitoa baraka kwa waumini na ibada iliongozwa kwa shukrani na furaha.
Uratibu wa Ugawaji wa Vitabu
Vitabu vya Position ya Kiha viligawiwa kwa wahumini waliokuwa wakitoka kanisani, kwa usimamizi wa watu waliokuwa milangoni. Kila mmoja kila mmoja alipokea kitabu/portion kwa mpangilio mzuri na bila msongamano, wakihakikishiwa upatikanaji wa Neno la Mungu katika lugha yao.
Furaha ya Waumini
Baada ya ugawaji wa vitabu hivi, waumini Walionekana wakifurahia vitabu vyao nje ya Kanisa. Walijawa na furaha kubwa huku wakimshukuru Mungu pamoja na viongozi wa mradi kwa jitihada zao kufanikisha kazi hii. Pia walipiga picha ya pamoja ya kumbukumbu wakiwa wameshikilia vitabu vyao.
Tukio hili lilifanikiwa kwa kiwango kikubwa, na waumini walionyesha kufurahia uzinduzi wa tafsiri hii mpya ya Biblia katika lugha yao ya Kiha, ikionyesha mwendelezo wa kazi nzuri ya Chama cha Biblia na Kanisa katika kukuza na kueneza Neno la Mungu kwa jamii nzima.
Dodoma, 03 Novemba 2024 – Maadhimisho ya kilele cha Juma la Biblia mwaka huu yamefanyika kwa mafanikio makubwa mkoani Dodoma, katika Uwanja wa Mashujaa. Maadhimisho hayo yaliyoanza na maandamano ya amani kutoka makao makuu ya Chama cha Biblia cha Tanzania (CBT) hadi viwanja vya zamani vya Mashujaa, yalivutia umati wa wanachama na wadau mbalimbali. Maandamano hayo yalipambwa na bendi ya tarumbeta na kwaya ya wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), huku wanachama wakivalia tisheti zilizo na nembo ya CBT na kauli mbiu ya mwaka huu: “Neno la Mungu, Maadili Yetu.”
Mgeni rasmi katika sherehe hizo alikuwa Askofu Amos Muhagachi, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa CBT, akiwa ameambatana na viongozi wengine wakuu wa Chama akiwemo Katibu Mkuu wa CBT, Dkt. Alfred Elias Kimonge, na Mkurugenzi wa CBT, Dkt. Anna Solo. Pia, sherehe hizo zilihudhuriwa na viongozi wa makanisa, wanachama wa CBT, na wanafunzi wa UDOM.
Katika hotuba yake mgeni rasmi Askofu Amos Muhagachi alisoma Neno la Mungu kutoka Zaburi 119:105, “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu,” akisisitiza umuhimu wa Neno la Mungu kama msingi wa maadili. Alisema, “Biblia ni kitabu kinachotuunganisha sisi Wakristo na kinatuonyesha maisha ya mwanadamu, ukombozi, na umilele wake.” Pia alihimiza mpango mkubwa wa maadhimisho mwaka ujao, kwa kushirikiana zaidi ili kufikia wadau wengi.
Katika hotuba yake, Katibu Mkuu Dkt. Kimonge aliwashukuru wanachama na wadau wote waliojitolea kushiriki Juma la Biblia lililoanza tarehe 28 Oktoba na kumalizika leo 03 Novemba. Dkt. Kimonge alieleza kwamba lengo kuu la CBT ni kutafsiri, kuchapisha, na kusambaza Biblia kwa watu wote, wakiwemo Wakristo na wasio Wakristo. Alihimiza umoja katika kuchangia kazi hii muhimu, hasa kwa makundi yasiyo na uwezo wa kununua Biblia, kama vile wafungwa na vijana.
Katika kuelezea historia ya CBT, Dkt. Kimonge alitaja hadithi ya binti Maria Jones, mwenye umri wa miaka kumi na tano, aliyekuwa mkulima wa Wales. Kiu yake ya kumiliki Biblia ilichochea harakati za kuanzisha vyama vya Biblia, ambavyo leo vinafanya kazi katika nchi zaidi ya 160, kusambaza mamilioni ya Biblia na maandiko mengine katika lugha zaidi ya 15,000.
Maadhimisho hayo yamehitimishwa kwa maneno ya shukrani kutoka kwa Meneja wa Mahusiano na Makanisa, Mch. Samweli Mshana, aliyewapongeza viongozi wote kwa kufanikisha Juma la Biblia kwa ufanisi. “Shukrani kwa viongozi wetu na wanachama wote wa CBT kwa kazi kubwa mliyofanya. Mungu awabariki sana,” alisema Mch. Mshana.
Maadhimisho ya Juma la Biblia yanaendelea kuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha ushirikiano kati ya waumini, wadau, na jamii kwa ujumla kupitia Neno la Mungu, na CBT inaahidi kuendelea na jitihada hizi kwa ustawi wa kiroho wa Watanzania.
Tukio la kihistoria la uzinduzi wa vitabu vya Biblia vilivyotafsiriwa kwa lugha ya Kinyiha vitabu vya Ruthu, 1 Samweli, 1 Wafalme, na Yona limefanyika leo katika Kanisa la Moravian Ushirika wa Igamba, Jimbo la Mbozi. Uzinduzi huu umefanywa na Katibu Mkuu wa Jimbo la Mbozi, Mchungaji Rayson Kibona, huku ukiongozwa na Mch. Lastone Chalotela Mwamlima ambaye ni mratibu wa mradi pia mwenyekiti wa wilaya na Mchungaji Wiliadi Zewanga mchungaji wa ushirika wa Igamba Moravian.
Tukio hilo muhimu limeandaliwa na Chama cha Biblia cha Tanzania kwa kushirikiana na makanisa ya Kikristo kutoka Mkoa wa Songwe, hasa Wilaya ya Mbozi ambako lugha ya Kinyiha huzungumzwa kwa wingi.
Katika hafla hiyo, viongozi mbalimbali walihudhuria na kutoa hotuba kuhusu umuhimu wa tukio hili. Madam Leah Kiloba, Meneja wa Tafsiri kutoka Chama cha Biblia cha Tanzania, aliwasilisha ujumbe wa Chama hicho na Umoja wa Vyama vya Biblia Duniani, akieleza majukumu makuu ya Chama kuwa ni kutafsiri, kuchapisha, na kusambaza Biblia kwa gharama nafuu ili kuwafikia watu wote. Kiloba alisisitiza umuhimu wa mradi huu kwa jamii ya Wanyiha na kuwashukuru washiriki wote waliotoa mchango katika tafsiri. Pia aliwaomba jamii ya wanyiha baada ya kupokea vitabu hivyo wavisome kisha kama kuna makosa wayalete ili yalekebishwe mapema kabla ya Biblia kamili kukamilika.
Watafsiri na Wahakiki wa Tafsiri
Kazi ya kutafsiri vitabu hivi imefanywa kwa bidii na ushirikiano wa wataalamu wa lugha, viongozi wa makanisa, na wahakiki wa tafsiri. Baadhi ya watafsiri wakuu ni:
– Mch. Lastone Chalotela Mwamlima (mratibu)
– Mch. Justus Vhalondeghe Sinkonde
– Mch. Philimon Partson Balanga
– Dada Christina Chares Singogo
Wahakiki wa tafsiri walioshiriki ni pamoja na:
– Mch. Sila Mwamwezi
– Mch. Sostini Mwansenga
– Mch. Wilhelm Mwakavanga
– Mch. Selemani Nkota
– Mch. Lameck Nzowa
– Mch. Nichorous Shonza
– Dada Martha Mwashiuya
– Dada Upendo Mwashilindi
Pia, Dkt. Chris Pekka Wilde alitajwa kwa mchango wake muhimu wa kiufundi kama mshauri wa mradi huu.
Uzinduzi huu ulihudhuriwa na wachungaji na viongozi wa makanisa kutoka madhehebu tofauti, wakiwemo wawakilishi kutoka makanisa ya Last Church, Kanisa Katoliki, TAG, na KKKT. Viongozi hawa walipongeza hatua hii kama ishara ya kuendelea kwa kasi kwa mradi huu, ambao unalenga kuongeza upatikanaji wa Biblia kwa lugha ya Kinyiha kwa ufasaha.
Tukio hili limeibua matumaini makubwa na linaashiria mwanzo mzuri kwa jamii ya Wanyiha kupata Biblia kwa lugha yao wenyewe, hatua ambayo itaimarisha zaidi imani na kueneza Neno la Mungu kwa undani zaidi katika eneo hilo.